Njia moja muhimu ya kuwalinda watoto dhidi ya hatari ya kifafa ni kuhakikisha ya kwamba wanapata chanjo zao kwa wakati unaofaa. BCG kwa mfano humlinda dhidi ya kifua kikuu. Ugonjwa wa kifua kikuu umekuwa ugonjwa wa kawaida hivi leo na unapoathiri mtoto mdogo ambaye hajapata chanjo, hatari ya kupata ugonjwa homa ya uti wa mgongo (meningitis) huongezeka. Homa ya uti wa mgongo itamweka mtoto kwenye hatari kubwa ya kupata kifafa. Chanjo zingine maalumu kwa aina tofauti za homa ya uti wa mgongo zinapatikana hospitalini lakini kwa ada.
Homa ni kitu kinachoongezea hatari ya kupatwa na mshtuko ilhali inaweza kudhibitiwa vyema. Mtoto ambaye homa yake inaruhusiwa kupanda juu yuko katika hatari ya kupatwa na mshtuko. Ni muhimu kwa homa kudhibitiwa vizuri pindi tu inapoanza. Udhibiiti wa homa unajumuisha; kutumia dawa kama Panado (paracetamol) ama Brufen (Ibuprofen), mtoe mtoto nguo kisha umpanguze na kitambaa kilicholoweshwa ndani ya maji yenye joto la kadri na la muhimu zaidi ni kutafuta msaada wa matibabu.
Ulinzi dhidi ya jeraha, haswa jeraha kwenye kichwa ambayo ndiyo sababu nyingine ya kifafa. Ulinzi hutokana na kuhakikisha ya kwamba watoto hawezi kuanguka kwa urahisi kutoka katika sehemu iliyo juu, usimamizi unaofaa wanapocheza na kuweka mbali vitu ambavyo vinaweza kuwaletea madhara wanapocheza. Unaposafiri kwenye gari, ni muhimu kutumia mishipi ya usalama ili kupunguza hatari ya kujeruhiwa ikiwa kutatokea ajali. Jeraha la kichwa ndilo jeraha ambalo hutokea mara kwa mara kukitokea ajali.